Mafuriko nchini Sudan Kusini yaathiri watu 893,000, zaidi ya 240,000 wakoseshwa makazi

1 week ago 12

Watu 893,000 wameathiriwa na mafuriko nchini Sudan Kusini na zaidi ya 241,000 kukoseshwa makazi, shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu (OCHA) lilisema Alhamisi katika ripoti iliyosahihishwa kuhusu janga hilo.

Mashirika ya misaada yalionya kwamba taifa hilo changa duniani, linalokabiliwa sana na athari za mabadiliko ya hali ya hewa, limekumbwa na mafuriko mabaya sana katika miongo kadhaa.

“Mafuriko yanaendelea kuathiri na kuwahamisha watu kwenye makazi yao kote nchini,” OCHA ilisema katika taarifa.

“Mvua kubwa na mafuriko yamekwamisha usafirishaji wa misaada kwenye barabara 15, na kufanya watu kushindwa kufika kwenye maeneo yaliyoathiriwa.”

OCHA ilisema watu 893,000 wameathiriwa na mafuriko katika kaunti 42 za Sudan Kusini kati ya kaunti 78, vile vile katika eneo la Abyei, eneo linalozozaniwa kati ya Juba na Khartoum.

Zaidi ya watu 241,000 wamehamishwa kwenye makazi yao katika kaunti 16 na eneo la Abyei” na kutafuta makazi kwenye maeneo ya juu”, OCHA iliongeza.

Source : VOA Swahili

SHARE THIS POST